Occupational Safety and Health Authority
  +255-22-2760548 / 2760552       info@osha.go.tz                     

JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA

WAKALA WA USALAMA NA AFYA MAHALI PA KAZI

Agenda Za Kimkakati


1.    Kupunguza ama kutokomeza kabisa ajali, magonjwa na vifo vitokanavyo na kazi katika sehemu za kazi kote Tanzania Bara. Ili tufike huko, ni lazima kila wakati tujiulize kama tunakidhi vigezo vilivyotumika kuanzisha chombo hiki. Ni lazima tujiulize maswali matatu muhimu: Je, sisi kama taasisi inayosimamia usalama na afya mahala pa kazi, ni kwa kiasi gani tunafanikisha lengo la kuanzishwa kwa taasisi yetu; Je, sehemu za kazi zikoje kiusalama na kiafya kwa wafanyakazi wanapokuwa kazini; na  Je, usimamizi wetu wa masuala ya usalama na afya ukoje? 
2.    Kuwajengea uwezo watendaji. Ili taasisi ya OSHA iweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi unaohitajika basi ni lazima kuhakikisha kwamba watumishi wake wana ujuzi na weledi unaohitajika ili kuleta ufanisi wa majukumu yao ya kila siku. Hivyo tutahakikisha kwamba tunawaendeleza watumishi wetu kwa kuwapa mafunzo na ujuzi unaohitajika wakati wote.
3.    Kupanua uelewa wa wadau wetu na wananchi kwaujumla kuhusu masuala ya Afya na Usalama mahali pa kazi. Ili kazi yetu iwe rahisi na yenye kuleta tija hatuna budi kuhakikisha kwamba wadau wetu na wananchi kwaujumla wa uelewa wa kutosha kuhusu umuhimu wa masuala haya katika maisha yao. Lengo hili tutalifikia kwa kujikita katika kuelimisha zaidi kuliko kuadhibu ili kupunguza ukiukwaji wa kanuni za usalama na afya mahala pa kazi na pale inapobidi kuwawajibisha waajiri kisheria. Hii itasaidia pia kuondoa mtazamo hasi dhidi ya OSHA na mambo ambayo taasisi hii inayasimamia.
4.    Kuandaa programu maalum ambazo ni endelevu kwa ajili ya usimamizi wa Usalama na Afya katika sekta isiyo rasmi yenye wafanyakazi walioajiriwa na waliojiajiri wenyewe. Sekta isiyo rasmi inakua kwa kasi kubwa sana na ina wafanyakazi wengi ambao hawafikiwi na huduma za OSHA. Programu zitakazoandaliwa zitakahakikisha kwamba wafanyakazi katika sekta isiyo rasmi wanafanya kazi katika mazingira yenye usalama na afya. Aidha zitajikita katika kusaidia utengenezaji wa ajira zenye staha pamoja ujengaji wa tabia ya kukusanya takwimu muhimu mahala pa kazi, zikiwemo za ajali, magonjwa na vifo, siku za kazi zilizopotea kutokana na ajali, mwenendo wa uzalishaji kabla na baada ya mafunzo na kuongezeka kwa uzingatiaji wa kanuni za usalama na afya mahala pa kazi.